Serikali ya Sudan Kusini imesusia raundi ya pili ya mazungumzo ya amani
yaliyoanza Jumatatu mjini hapa chini ya upatanishi wa Jumuiya ya
maendeleo kwa nchi za pembe ya Afrika (IGAD).
Awamu ya pili ya mazungumzo hayo ilitarajiwa kuanza baada ya kusainiwa
kwa mkataba wa kukomesha uadui katika nchi hiyo. Mkataba huo umekosolewa
vikali huku kukiwa na ripoti ya ukiukwaji kwa pande zote mbili
zinazohasimiana, kila upande ukirusha lawama kwa upande mwingine.
Watu waliohudhuria mkutano huo wamesema jaribio la serikali kutaka
kuzuia mchakato huo lilipingwa na mkutano ulianza bila uwakilishi wao.
"Sisi tuliitwa kwenye ukumbi wa mkutano na tulipoingia tuligundua kuwa
ujumbe wa serikali haukuwepo. Tuliwauliza wajumbe wa timu ya usuluhishi
na tuliambiwa kuwa ujumbe wa serikali ulikuwa unahitaji uwakilishi
zaidi," kilisema chanzo kilichohudhuria mkutano huo.
Vyanzo hivyo vinasema wajumbe wa timu ya serikali walisema wanahitaji uwakilishi mkubwa kwa sababu kuna umuhimu sana kwao.
Wapatanishi wa IGAD walitenga viti 12 kwa ajili ya timu ya serikali, idadi sawa na makundi mengine.
"Tuliomba watukubalie kwani tulikuja kwa sababu kila mmoja wetu katika
msafara huu alikuwa na ujumbe uliomfanya achaguliwe na serikali kuja,"
alisema ofisa wa serikali ambaye alipendelea kutokujulikana jina.
Maofisa wa serikali wanasema timu yao itarejea kuendelea na mazungumzo mara baada ya matakwa yao kutekelezwa.
Post a Comment