0
Watu kumi na wawili wamekufa maji na wengine 27 wamejeruhiwa na idadi isiyofahamika hawajulikani walipo baada ya chombo walichokua wakisafiria kilichotambuliwa kuwa jahazi Mv Burudan au Sayari kutoka Tanga kwenda Kaskazini Pemba kukumbwa na dhoruba na kuzama Baharini.

Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi mkoani Tanga Benedict Wakulyamba amesema ajali hiyo imetokea majira ya saa saba usiku januari 10 ambapo taarifa za awali zimeeleza kuwa kuwa ajali hiyo imetokana na dhoruba na upepo mkali.

Wakulyamba amesema jeshi la Polisi kwa kushirikiana na jeshi la wananchi pamoja na zimamoto wapo eneo la tukio kusaka miili na majeruhi ambao idadi yao bado haijajulikana.

Kwa upande wake kaimu Mganga mfawidhi wa Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Tanga Bombo Dkt Godluck Mbwilo amethibitisha kupokea majeruhi 25 na miili 12 ambpo ndugu na jamaa wanaendelea na zoezi la kuwatambua ndugu zao.

Baadhi ya majeruhi waliolazwa katika hospitali ya Bombo wameeleza kuwa kabla ya ajali ulivuma upepo mkali ambapo chombo kilianza kuyumba na kupoteza mwelekeo kabla ya kupasuka na kuzama.

Jahazi hilo lililozama limesajiliwa Pemba kwa namba Z5512 linamilikwa na Suleiman Bwimbi.

Post a Comment

 
Top